Monday, February 17, 2014

SERIKALI KUSHUSHA BEI YA VING'AMUZI

Serikali imesema inatarajia kuwa kodi ya ving'amuzi itashuka ili kuhamasisha kampuni nyingi zaidi kujitokeza kuuza vifaa hivyo kwa wananchi, tofauti na sasa.

Hayo yalisemwa mjini hapa mwishoni mwa wiki na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, wakati  akifunga mkutano wa jukwaa la kujadili mchakato wa kuhama kutoka mfumo wa analojia kwenda digitali, uliohusisha nchi zaidi ya 25 duniani.

"Bei za ving'amuzi ipo chini japo sisi serikali tunaona bado ipo haja tupunguze kodi zaidi ili ishuke chini zaidi kwa ajili ya kuwezesha makampuni mengi kununua vifaa hivyo na kuwauzia wananchi hasa waliopo vijijini," alisema.

Aidha, Naibu Waziri huyo alisema ni nia ya serikali kuona vijana wengi wanawezeshwa kwa kujikusanya kwenye vikundi vyenye uwezo wa kutengeneza vipindi vya televisheni na makala ili waweze kujiingizia kipato.

Alisema kabla ya Tanzania kuingia katika mfumo wa dijitali, wamiliki wengi wa televisheni ndiyo waliokuwa wanatengeneza vipindi na makala mbalimbali kwenye vituo vyao, lakini kwa sasa baada ya mfumo huo kuanzishwa kuna fursa ya vijana kutengeneza wenyewe vipindi hivyo.

"Kilichopo hapa vijana wajiendeleze ili wawe na ujuzi wa kutengeneza makala na kuandaa vipindi ambavyo vitatumika kwenye vituo vya televisheni na hatua hii itawawezesha kupata fedha za kutosha," alisema.

Alisema moja ya maazimio ya mkutano huo ni kuona bei za televisheni zinashuka zaidi ili wananchi wengi wamudu kuzinunua kwa ajili ya kujipatia habari za dunia zinazoendelea na masuala mengine mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA),

Profesa John Nkoma alisema mfumo wa dijitali umesaidia wananchi kwa upande wa simu za viganjani kuwasiliana na mtu yoyote kwa njia mbalimbali zilizoko kwenye simu hizo.

"Haya ni matunda ya dijitali na maendeleo yamekuwa makubwa sana katika utumiaji wa simu hizi, kama vile wengi wanawasiliana kwa Wa-tsap, lakini kwa upande wa televisheni ni ngumu kidogo kuingia maeneo yote kwa mara moja," alisema.

Profesa Nkoma alisema awamu ya pili ya uzimaji wa mitambo ya analojia itakuwa katika mikoa ya Morogoro, Tabora, Musoma, Mara na Dodoma na ifikapo Juni 2015 nchi nzima itakuwa imeingia katika mfumo wa dijitali kama makubaliano ya Geneva yanavyosema.

Kuhusu  uvumi wa kwamba mfumo huo unauwa televisheni za zamani, alisema ni kitu cha kupuuza kwani hakina ukweli, kwani kitu kinachotakiwa ni kununua king'amuzi na mhusika ataendelea kupata matangazo ya televisheni kama kawaida.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment