Tuesday, July 22, 2014

MKE WA POLISI AFIA NYUMBANI KWA MWENDESHA BODABODA


Jeshi la Polisi linamshikilia dereva mmoja wa pikipiki, maarufu kama bodaboda wilayani Mwanga mkoani Kilimanjaro baada ya mke wa askari polisi kukutwa amekufa chumbani kwa dereva huyo. 
 
Tukio hilo ambalo limezua gumzo kubwa wilayani humo lilitokea juzi saa 12:00 jioni katika eneo la New Mwanga wilayani humo na mtuhumiwa akidaiwa kukutwa akiwa amelewa chakari.
 
Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, Shaibu Ndemanga amethibitisha kuwapo kwa tukio hilo na kusema uchunguzi unaendelea.
 
“Hilo tukio lina ukweli na bahati mbaya sana mumewe ndiyo kwanza amehamishiwa Geita na alikuwa akaripoti halafu aje kuchukua familia yake,” alisema Ndemanga.
 
Mkuu huyo wa wilaya ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo, alisema hadi sasa haijafahamika nini kilitokea na kwamba hilo ni moja kati ya mambo ambayo polisi inachunguza.
 
“Hayo yote kwamba ilikuwaje akawa chumbani kwa huyo kijana, nini sababu za kifo yatajulikana kadiri upelelezi unavyoendelea,” alisema.
 
Imeelezwa kuwa jana ilikuwa siku ya askari huyo kuripoti katika kituo chake kipya cha kazi.
 
“Mpaka sasa hivi haijajulikana nini hasa kilitokea huko chumbani na ilikuwaje akawa chumbani kwa huyo dereva,” alisema mmoja wa watu waliokuwapo katika eneo la tukio ambaye hata hivyo, hakutaka kutaja jina lake na kuongeza kuwa jana saa sita mchana, mwili wa mwanamke huyo ulichukuliwa kutoka Hospitali ya Wilaya ya Mwanga na kuhamishiwa Hospitali ya Rufaa ya KCMC kwa uchunguzi.
 
Taarifa za awali zinasema kuwa mwili wa marehemu ulikuwa na mikwaruzo shingoni hali inayotia shaka kuwa huenda alinyongwa.
 
Habari nyingine zinadai kuwa siku ya tukio, mwanamke huyo alikuwa ameaga kuwa anakwenda kanisani lakini baadaye simu yake ilipopigwa ilikuwa ikipokewa na mwanamume.
 
Ilidaiwa kuwa mume wa marehemu alipojaribu kupiga simu ya mkewe, ilikuwa ikipokelewa na mtu aliyeonekana kuwa ni mlevi wa kupindukia hali iliyomtia wasiwasi na kuamua kuwapigia simu marafiki zake wa karibu ili wamsaidie kumtafuta ndipo walipopata taarifa kuwa ulikuwapo uhusiano kati ya shemeji yao na dereva huyo wa bodaboda.
 
Ilidaiwa kuwa marafiki hao walikwenda moja kwa moja nyumbani kwa dereva huyo wa bodaboda ambako walimkuta akiwa amelewa na walipoingia ndani walimkuta shemeji yao akiwa ameshafariki dunia.

Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz hakupatikana jana kuzungumzia tukio hilo kwa kuwa alikuwa kwenye ziara ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda huko Gonja wilayani Same. 

Credit: Mwananchi

WAKAMATWA WAKIWA NA MABOMU 7 RISASI 6 NA BARUTI JIJINI ARUSHA



JESHI la polisi hapa nchini limefanikiwa kuwatia mbaroni vinara wa milipuko ya mabomu hapa nchini, Yusufu Ally (30) na mkewe Sumaina Juma (19), wakazi wa Sombetini, wakiwa na mabomu ya kurusha kwa mkono aina ya Gurnet saba, risasi sita za shotgun, baruti, mapanga mawili na bisibisi moja. 

Mtaalamu wa mabomu kutoka Jeshi la Polisi akionyesha kwa waandishi wa habari moja ya bomu lililokamatwa.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Isaya Mngulu, alisema kati ya mabomu hayo moja limetengenezwa nchini Ujerumani na sita yametengenezwa Urusi.
 
Alisema watuhumiwa hao walikamatwa jana saa 2 usiku katika eneo la Sombetini mjini hapa baada ya jeshi la polisi kupata taarifa juu ya watuhumiwa hao kuhusika na matukio ya milipuko ya mabomu.
 

 
Aliongeza kuwa polisi inamtafuta kinara muhimu wa mabomu, Yahaya Hussen Hela (35), mkazi wa Mianzini jijini hapa, huku watuhumiwa wengine 25 akiwemo mfanyabiashara maarufu jijini hapa anayemiliki mabasi ya Kandahal Said Temba (42), pamoja na Imamu wa Msikiti wa Masjidi Qubia, Japhal Lema (38) ambaye pia ni mwalimu wa shule ya msingi wilayani Arumeru wakishikiliwa kuhusisana  matukio ya mabomu.
 
Miongoni mwa watuhumiwa hao, sita kati yao wanahusishwa na tukio la ulipuaji wa mgahawa wa Vama uliotokea Julai 7, mwaka huu,na kusababisha majeruhi wanane raia wenye asili ya Kiasia.
 

Watuhumiwa sita wa mlipuko huo wametajwa kuwa ni Shabani Hussen (38)ambaye alikuwa mlinzi katika mgahawa huo, Mohamed Nuru (30) mlinzi wa mgahawa wa jirani na tukio, Japhari Lema (38), Abdul Mohamed (31), wakala wa mabasi stand pamoja na Said Temba (42), wote wakazi wa jijini Arusha.
 
Mngulu alisisitiza kuwa polisi inaendelea kuwasaka wahuhumiwa wengine zaidi na kwamba jeshi hilo limeahidi kutoa zawadi kwa atakayeweza kutoa taarifa za siri zitakazowezesha kupatikana kwa wahusika hao.


Credit: Global publisher.